Wataalamu walioangalia tafiti nyingi zilizofanyika kuhusu nyama nyekundu (red meat) na saratani wameona upo uthibitisho wa kutosha (mkubwa) kwamba ulaji wa nyama nyekundu kwa kiasi kikubwa unaongeza uwezekano wa kupata saratani ya utumbo mkubwa (colorectal cancer) (WCRF 2007). Tafiti hizo zimeonyesha kula hadi nusu kilo kwa wiki haiongezi uwezekano wa kupata saratani, lakini kila gramu 50 inayoongezeka huongeza uwezekano wa kupata saratani kwa asilimia 15 (15%).
Nyama nyekundu ni nyama ya ng’ombe, mbuzi, kondoo au nguruwe. Ni vema kuelewa hilo maana nimewahi kukutana na watu wanaodhani nguruwe sio nyama nyekundu. ukweli ni kwamba nguruwe ni nyama nyekundu. La muhumu hapa ni kupunguza kiasi cha nyama nyekundu tunachokula kwa wiki, na kuongeza zaidi ulaji wa mboga mboga, matunda na vyakula vinavyotokana na mimea, kama mikunde (legumes), bila kusahau nafaka zisizokobolewa sana (kama dona). Mazoezi ya mwili pia yawe sehemu ya mkakati wako wa kupunguza uwezekano wa kupata saratani.
Jipende! Ufunguo wa mtindo bora wa maisha upo mkononi mwako.








