Katika matunda yenye vitamin C kwa wingi, ubuyu ni mojawapo. Tunda hili pamoja na virutubishi vingine, lina vitamin C kwa wingi sana lakini hata pale tunda hili linapopatikana halitumiki ya kutosha. Tunapozungumzia “kula matunda kwa wingi kila siku”, ubuyu unaweza kuwa sehemu ya matunda hayo. Pia ubuyu unaweza kutumika kutengeneza kinywaji kwa kutumia unga wake kuchanganya na maji yaliyo safi na salama. Ubuyu pia unaweza kuchanganywa kwenye uji ambapo unaongeza ladha na virutubishi hasa vitamin C.

Tunda hili wakati mwingine husahaulika na hata kudharauliwa, hasa pale linapopatikana kwa urahisi mno, na wakati mwingine hata bila kununua. Kwa bahati mbaya sana matunda ambayo wakati mwingine tunayaita matunda pori, yameonekana kama matunda ya hali ya chini, au yasiyo na hadhi. Hali hii tunahitaji kuibadili kwani tunda kama ubuyu au pia ukwaju na matunda pori mengine ni matunda mazuri sana, na inafaa tuyatumie kama sehemu ya matunda pale yanapopatikana, na hasa wakati wa msimu wake.
Tutumie matunda haya kutengeneza vinywaji kwa ajili ya familia. Kutumia ubuyu pamoja na mlo husaidia kuongeza ufyonzwaji wa madini ya chuma kutoka katika chakula kilicholiwa hasa pale tunapotumia vyakula vitokanavyo na mimea. Hii ni kwa sababu ubuyu una vitamin C kwa wingi, na vitamini C huhitajika ili kuongeza ufyonzwaji wa madini ya chuma kutoka kwenye mlo huo. (Madini ya chuma huongeza damu mwilini). Hivyo ni muhimu kwa kila mtu kufanya matunda sehemu ya mlo, ukiwepo ubuyu, na hasa wanawake wajawazito ambao wana hatari kubwa zaidi ya kupata upungufu wa damu.
UBUYU………….. tulienzi tunda hili! tulitumie! tuliongezee hadhi! Tulifaidi! Tule matunda kwa wingi kila siku.
Jipende: Ufunguo wa mtindo bora wa maisha upo mkononi mwako.








April 12th, 2010 at 3:58 pm
Ahsante mama Mary Materu kutukumbusha na kutupa hamasa ya umuhimu wa kula matunda katika kila mlo na haswa matunda ambayo wengi wetu mara nyingi hatuzingatii au hatutambui thamani kubwa ya vyakula hivyo kwa ajili ya lishe na afya ya miili yetu. Kwa uzoefu ubuyu unaonekana km ni tunda kwa watoto.Nadhani ni wakati muafaka kuondoa hii fikra. Mbali na kutengeneza kinywaji au kuchanganya ktk uji, unga wa ubuyu unaweza kuongezwa ktk juisi za matunda mengine km maembe, parachichi, papai na mengineyo na hata ktk kuongeza ladha ya vyakula.Hivyo ni rahisi sana kulitumia tunda la ubuyu ili kuboresha mlo.Nakushukuru kwa kutupa taarifa yenye kutukumbusha na kutuhabarisha umuhimu wa matunda katika mlo na haswa tunda la ubuyu.